Fahamu Kuhusu Sumu Kuvu ni Janga La Afya kwa Mifugo - MifugoVets

SUMU KUVU (AFLATOXIN) KWENYE VYAKULA VYA MIFUGO :

Sumu kuvu ni sumu zitolewazo na aina ya ukungu kuvu (fangasi) unaoota kwenye mbegu za nafaka na jamii ya kunde, mazao ya mizizi, karanga, vyakula na malisho ya wanyama vikiwa shambani au kwenye ghala.

Ingawa aina nyingi za kuvu zinaweza kuota na kukua katika vyakula hivi, ni wachache tu amabao hutoa sumu kuvu. Aina hii fangasi kitaalamu hujulikana kama Aspegillus flavus na husambaza sumu kuvu ijulikanayo kama Afl atoxins.
Sumu hii huingia mwilini kwa binadamu au mifugo kupitia matumizi ya chakula kinachotokana na nafaka kama ya zao hili. Sumu kuvu haionekani kwa macho, haina harufu, haina kionjo, wala rangi, lakini kuvu anayetoa sumu hizo anaweza kuwa na rangi ya kijani, chungwa, kijivu au njano chafu na anaweza kutoa harufu ya uvundo. Karibia asilimia 25 ya vyakula ulimwenguni vina maambukizi ya sumu kuvu na watu bilioni 2.5 wako katika hatari ya kudhurika.

ATHARI YA SUMU KUVU:
Kwa kuwa sumu hii huchafua mazao kwa sasa inachukuliwa kama ni chanzo kikuu cha saratani ya maini kwa binaadamu. Sumu hii pia huharibu mfumo mzima wa kinga za mwili kwa binadamu na wanyama na hivyo kusababisha kushambuliwa kirahisi na magonjwa mbalimabali.

ATHARI NYINGINEZO ZISIZO BAYANA:
Kadhalika watafiti kutoka Taasisi ya International Institute of Tropical Agriculture (IITA) Benin, Afrika ya Magharibi wameweza pia kuielezea sumu hii kuwa ni chanzo kikubwa cha kuzorota kwa ukuaji wa viumbe mbalimbali. Mathalani ni sababu kubwa ya kuzorota kwa ukuaji wa watoto katika ukanda huu wa Afrika.
Baadhi ya watoto hupata sumu hii katika umri mdogo na matokeo yake kasi ya ukuaji wao hupungua kwa kiasi kikubwa na hali hii hudhihirika pale watoto hawa wanapoachishwa maziwa ya mama na hasa wanapokuwa kwenye hatari za maambukizi ya magonjwa mengine kama kichocho, kuhara, malaria na magonjwa ya mfumo wa hewa, anabainisha Dr. A. Haunsa wa Taasisi ya IITA.

ATHARI KWA BINAADAMU:
Changamoto ya sumu kuvu ni kwamba si rahisi kwa mara zote mkulima kuweza kutambua aina ya fangasi wanaozalisha sumu hii kwenye nafaka anazolima. Na Zaidi ya hapo sumu hii si rahisi kuitambua kwa macho au kuweza kutoweka kwenye chakula kwa kupika au kuchachusa vyakula hivi.
Hivyo upo uwezekano kwamba idadi kubwa ya watu Afrika Mashariki kuwa wameathiriwa na sumu hii sugu kama ilivyo kwa nchi za Afrika
Magharibi japokuwa takwimu kamili za ukubwa wa athari hii haijawekwa bayana. Vilevile walaji wengi hawana habari kwamba wanatumia vyakula vilivyochafuliwa na sumu kuvu na hata wale ambao wananunua vyakula vyao kwenye maduka makubwa hawakusalimika na sumu hii anasema, Dr. George Siboe Mhadhiri wa Chuo Kikuu Cha Nairobi aliyefanya tafi ti iliyoweza kubaini sumu kuvu kwenye bidhaa mbalimbali maarufu za unga zinauzwa kwenye maduka mbalimbali.

MAINI YA KUKU WA NYAMA

NINI HASA CHANZO CHA SUMU KUVU?
Tafiti mbalimbali zimeonysha kuwa Kwa kiasi kikubwa wadudu ndio hasa wanaochangia kusambaa kwa sumu kuvu kwenye mahindi na nafaka zingine mashambani. Hii inamaanisha kwamba uwepo wa idaidi kubwa ya wadudu kama kombamwiko na kipukusa kwenye maghala ya chakula hukaribisha uwezekano mkubwa wa tishio la janga la sumu hii.
Kwa mfano huko Afrika Magharibi imegundulika kwamba tatizo la sumu kuvu huanzia mashambani mathalani, uharibifu unaofanywa na dumuzi kwenye mazao yaliyokomaa shambani huongeza uwezekano wa nafaka kuathiriwa na jamii ya fangasi ijulikanayo kama ukungu na hatimaye husababisha kusambaa kwa sumu kuvu ambayo huzidi kuongezeka kadiri mashambulizi ya mdudu dumuzi yanavyoongezeka. Hii inamaanisha kudhibiti wadudu hawa mashambani kwa kutumia njia za kibaolojia ndiyo suluhu ya kudumu dhidi ya janga la sumu kuvu.

NJIA ZA KUDHIBITI MAAMBUKIZI YA SUMU KUVU:
• Lima aina za mazao zenye ukinzani dhidi ya kuvu wanaotoa sumu kuvu (kama aina hizo zinapatikana)
• Vuna mazao yakiwa yamekauka vizuri kama inavyoshauriwa na wataalamu na epuka kutia majeraha kwenye mazao yako
• Usianike mazao yako kwenye udongo mtupu. Anika sehemu iliyoinuka kama meza na utumie turubai au aina nyingine ya kifaa cha kuanikia
• Wakati na baada ya kuvuna tupa mbegu au mazao yaliyooza
• Hifadhi mazao mahali pakavu na pasipo na joto. Hakikisha mazao yaliyohifadhiwa hayalowi
• Ghala liruhusu mzunguko wa hewa, zuia wadudu waharibifu na kuvu kwa kunyunyiza madawa yaliyokubalika na kushauriwa, kwa uhakika zaidi tumia”SRERIFUM” hasa kwenye mahindi na maghala ya kuhifadhia nafaka.
• Kama yanapatikana, tumia madawa ya kibayologia kama vile Afl aSafeTM (aina ya kuvu ambaye hukinzana na yule atoaye sumu kuvu). Tumia madawa yanayodhibiti na kuondoa sumu kuvu wakati wa usindikaji wa vyakula vya binadamu kama vile mycobind kwa upande wa wanyama.

MTIRIRIKO WA SUMU KUVU:
Kwa tafsiri fupi na ya haraka ya mchoro huu hapo juu, unaonyesha mlaji wa bidhaa zitokanazo na mifugo na kilimo ndiye mhanga mkubwa wa madhara ya sumu kuvu. Mlaji huyu huweza kuathirika aidha kwa kula moja kwa moja mazao kama mahindi yaliyoathirika au maziwa ya ng’ombe aliyepata sumu kuvu kupitia kulishwa malisho yaliyo na sumu hii.
Hata hivyo ni huyuhuyu mlaji ndiye anayezipa uhai sekta nzima hizi za uzalishaji kupitia mapato ya mauzo ya bidhaa hizi kwake. Hivyo kuna haja ya kumhakikishia usalama wake (Consumer protection) ili kuweza kuzinusuru sekta hizi za uzalishaji kwani kama ataangamia basi wadau wote kwenye mnyororo wa uzalishaji wataathirika pia.

ATHARI YA SUMU KUVU KWA MIFUGO YETU:
Kama ilivyo kwa binaadamu mifugo yetu kama ng’ombe na kuku inapotumia vyakula vilivyoathiriwa na sumu hii kushindwa kukua vyema na hatimaye kushindwa kutoa mazao mazao bora na kwa wingi. Vilevile upo uwezekano wa sumu hii kusambaa kwa binaadamu kupitia utumiaji wa mazao yatokanayo na wanyama hawa.

NAMNA YA KUEPUSHA KWENYE MIFUGO:
Tumia vichanganyio (premix) ambavyo vinavyosaidia kuondosha sumu hii kwenye vyakula kwa ajili ya mifugo yetu. mmojawapo wa vichanganyio hivyo ni Mycobind na Farmacid Premix ambayo huchanganywa kwenye chakula cha mifugo kabla ya kupewa mifugo. Hii inapatikana kwenye maduka ya Farmers Centre na Farmbase pamoja na wakala wake wote nchini.

HITIMISHO:
Kutokana na madhara ya afya yanayosababishwa na sumu kuvu kwa binadamu na wanyama sumu kuvu haziruhusiwi kuwepo katika mazao yaliyokusudiwa kwa matumizi ya binaadamu, mifugo, biashara na kama uwepo wake ukigundulika mazao hayo ya kilimo hayataruhusiwa kuuzwa na baadaye yatateketezwa.Kwa kiwango kikubwa sumu kuvu huathiri biashara, faida na afya za wazalishaji na watumiaji kwa ujumla

0/Post a Comment/Comments

Previous Post Next Post

Download App

Sidebar Ads

Download App

Sidebar Ads